Kwa mujibu wa Shirika la Habari la Hawza, Katika maelezo yake, Mgalilaya amesema kuwa; wananchi wa Iran hupima uzalendo wa viongozi wao kupitia namna wanavyowahudumia wananchi katika sekta muhimu kama afya, elimu, maji, umeme, usafiri na upatikanaji wa chakula. Kwa mujibu wake, licha ya Iran kukabiliwa na vikwazo vya kimataifa kwa takribani miaka 47, huduma hizo bado zinapatikana kwa gharama nafuu na kwa uhakika.
Ameongeza kuwa; kwa mtazamo wake viongozi wa Iran hawaishi maisha ya anasa wala kujilimbikizia utajiri mkubwa. Akitoa mfano wa Imam Shahidi Ayatullah al-Udhma Sayyid Ali Khamenei (ra), mwandishi huyo amesema kuwa; baada ya kufariki kwake aliacha vitabu vyake pekee, na kwamba hakuwa hata na nyumba ya kumiliki, kwa mujibu wake hali hiyo inaonyesha maisha ya kawaida, ya kujisitiri na ya kujiepusha na kujilimbikizia mali aliyoyaishi kiongozi huyo.
Mgalilaya amesema kuwa; uzalendo unaoonekana miongoni mwa wananchi wa Iran umetokana na viongozi wanaojitolea kwa dhati kulitumikia taifa lao, si kwa kauli pekee, bali kwa vitendo vinavyojidhihirisha kupitia mipango ya maendeleo ya muda mrefu na sera zinazolenga kuboresha maisha ya wananchi.

Kwa mujibu wa mwandishi huyo, matumizi ya rasilimali za taifa kwa manufaa ya wananchi vimechangia kwa kiasi kikubwa kuimarisha imani ya wananchi kwa serikali yao. Amesisitiza kuwa; uaminifu huo haukujengwa kwa miujiza, bali kwa matendo yanayoonekana katika maisha ya kila siku ya wananchi.
Mwandishi huyo alihitimisha kwa kueleza kuwa; uzoefu alioupata nchini Iran umempa mtazamo mpya kuhusu uongozi, uzalendo na nafasi ya viongozi katika kujenga taifa lenye mshikamano, maendeleo na imani ya wananchi wake.
Zungu Mgalilaya
13 Julai 2026 / 21 Tir 1405 H.Sh.


Maoni yako